#4.
Mazoea Matatu Muhimu kwa Mahojiano Salama

WAPE WAATHIRIKA KUZUNGUMZA KWA NJIA WANAYOTAKA NA KWA WAKATI WANAOTAKA

Wakati wa ukatili wa kijinsia, wahalifu huchukulia watu kama vitu - sio kama watu ambao wana uwezo wowote juu ya kile wanatendewa. Je! unaweza kubadilisha mtizamo huo na kuwapa wahojiwa nafasi ya kujieleza?

Uhitaji wa kuwatendea watu walio katika mazingira magumu kwa uzingativu, heshima na hadhi inapaswa kuwa kitu cha wazi. Lakini hiyo inahusisha nini katika njia inayofaa? 

Kama mwanahabari anayehoji mhasiriwa, uko katika nafasi ya nguvu - hata kama huhisi hivyo. Maswala yatakuwa kuhusu uaminifu na usalama wa kihisia. Kwa hivyo, ni muhimu usifanye chochote ambacho kinaweza kumkumbusha mhasiriwa ukatili uliotekea hata kwa njia ndogo kama vile kuwaharakisha au kushinikiza majibu. Hii inaweza kuwa rahisi kupuuza wakati ni mfupi ukiwa katika eneo lenye hatari. 

Kwa hivyo, panga wakati wa kutosha wa mazungumzo na hakikisha kwamba mtu anayehojiwa anajua haya:

  • Hawajibiki kujibu maswali yoyote ambayo hangependa kusema.
  • Ni sawa kusimisha mahojiano wakati wowote.
  • Kwamba hutachapisha maelezo yoyote ambayo mhasiriwa anakuomba usichapishe.

Muone anayehojiwa kama mtu kwanza - na pili tu kama chanzo na nyenzo ya adithi yako.

Mahojiano ya vyombo vya habari yanaweza kusababisha madhara kwa wahasirika ikiwa ni mahojiano hayo yanafanywa kwa njia ya ukandamizi au bila kuzingatia usalama. Sehemu hii inazungumzia misingi ya mahojiano yanayofaa; namba #5 inaangalia kwa undani zaidi athari maalum za kiwewe na changamoto zake wakati wa kufanya kazi na wahasiriwa.

Mara nyingi, wanahabari wana wasiwasi kuwa kitendo cha kuzungumza juu ya visa vya kuumiza na vurugu kama vile ukatili wa kijinsia au mateso inaweza kusababisha madhara kwa anayehojiwa. Wanahabari wanaweza kuogopa kuwa wanawakumbusha wahasiriwa mambo ambayo ni afadhali kunyamaza. Au wanaweza kulinganisha shida ambayo mtu hupata wakati wa kusimulia hadithi yao na kusababisha madhara mapya.

Wataalam wengi wanaoshughulikia mambo ya kiwewe wanaofanya kazi na wahasiriwa wa ukatili wa kijinsia hawaoni kwamba kitendo cha kuongea kwa kivyake ndio chanzo cha hatari. Inahusiana zaidi na jinsi mhojiwa anavyojisikia salama wakati wa mazungumzo, na namna gani ana uwezo juu ya kile kinachozungumzwa, na pia jinsi kisa chake kitachapishwa baadaye [angalia #7 na #8]. Madhara yanaweza kutokea wakati watu wanahisi kuhukumiwa, kutosikilizwa, au kuhisi kuwa wanatumiwa kwa malengo mengine kama vile kupata habari ya kuuzika. Katika mahojiano ya masuala yanayohusiana na kiwewe, uaminifu ni kitu laini ambacho kinaharibika kwa urahisi.

Kuna wakati mwingine haitoshi kufikiria kwamba kuzungumza peke yake haitaleta madhara. Kwa mfano, ikiwa mtu amepitia jambo la kufedhehesha sana wakati wa zamani na kusahau matukio hayo na hawajawahi chunguzwa hapo awali – kama unyanyasaji wa kijinsia wa watoto, basi kuongea kuhusu tukio hilo inaweza kuamsha hisia mbaya na kuleta hatari tofauti. Kwa ujumla, kuwa mwangalifu usiwape habari za kushangaza na zisiyotarajiwa.

Jinsi ya kufanya mchakato kuwa wa kushirikiana zaidi kuliko kuonekana kutafuta habari tu 

Watu waliopitia ukatili wa kijinsia huhisi kama wamepoteza udhibiti wao- kitu ambacho kiliwapata ambacho hawakuwa na uwezo wa kuzuia. Njia moja ya kukabiliana na jambo hili ni kumpa mtu udhibiti ambao unaweza kutumia kama mwanahabari na kumshirikisha mhojiwa wako katika maamuzi juu ya mchakato huu. Hata mamuzi madogo yanaweza kuleta mabadiliko makubwa. 

Kabla ya kuanza mazungumzo unapaswa: 

  • kukiri kuwa wakati mwingine inaweza kuwa vigumu kuzungumza
  • wahusishe kikamilifu katika uamuzi kuhusu wapi wangependa kuhojiwa
  • ni saa gani ya siku ambayo ingewafaa zaidi – ni lini wangeweza kuwa na nguvu zaidi kwa mahojiano na wangependa kuongea kwa muda ga ni?
  • Je, kuna mtu yeyote ambaye angependa kuwa pamoja nae kwenye chumba kama vile rafiki au jamaa?
  • muulize ikiwa kuna kitu chochote ambacho hangependa wasizungumzie
  • na uwahakikishie kuwa sio lazima kujibu kile ambacho hawataki

Ni ada nzuri kuuliza watu kabla ya kuanza mazungumzo jinsi wewe kama mhojiwa utakavyotambua vipi hawataki kuongea zaidi na wanataka kusimamisha mazungumzo. Katika hali ya kuhadithia kisa watu wanaweza kujisahau. Kwa kuongezea, wengi wetu tunakuwa na hamu kubwa ya  kuendelea kuongea ili kumpendeza mtu anayeuliza maswali. Wanaweza kuwa sio wazuri sana kuashiria wakati wamechoka au wakati mazungumzo yameingia katika mada ambayo hawangependa kuzungumzia na kuwafanya wahisi vibaya. Kuangazia hili kabla ya mahojiano kuanza – na labda kukubaliana kwa ishara maalum – hufanya kupendekeza mapumziko au kubadilisha mada iwe rahisi bila usumbufu. 

Makubaliano kuhusu maneno ya kutumia

Sehemu ya #7 inazungumza zaidi juu ya chaguzi za lugha wakati wa kuchapishwa. Wakati wa mahojiano yenyewe, hakikisha kuwa unatumia maneno ambayo mhojiwa anaridhika nayo. Huenda kutumia misamiati inayotumiwa na wenyeji isiwe na manufaa. Kuna sheria zilizo wazi. Kwa mfano, haifai kamwe kumuita mhalifu kama mpenzi wa mtu. 

Watu wengi ambao wamepitia ukatili wa kijinsia wanajielezea kama ‘manusura’; lakini wengine wanaweza kuhisi kuwa “mhasiriwa” ni neno sahihi zaidi; na wengine wangependa kuepuka yote mawili. Ikiwa una shaka juu ya maneno gani ya kutumia, muulize mhojiwa wako nini angependelea. Kwa ujumla, ni muhimukila wakati kuheshimu jinsi watu wanajitambua.

Nguvu ya kusikiliza

Wakati watu wanaamini wanasikilizwa, wanajisikia salama zaidi na wanaweza kuongea kwa ufanisi zaidi. Kujua jinsi ya kusikiliza vizuri labda ni ujuzi muhimu zaidi ambaambao mwanhabari anahitaji wakati wa mazungumzo na mhasiriwa. Hii ni pamoja na kutoa nafasi kwa mhojiwa na kuuliza maswali rahisi na yaliyo wazi ambayo humpa mtu chaguo  ya jinsi wanataka kujibu lakini sio wazi sana kiasi kwamba inawalemea kujibu. 

Kumbuka kwamba kama ilivyojadiliwa katika sehemu ya #2 kutafuta idhini ni mchakato unaoendelea na sio tukio la wakati mmoja. Na kwa hivyo unaweza kutaka kutanguliza swali, Je! ni sawa kuuliza kuhusu ... (mada maalum au tukio). Kisha, mpe mhojiwa nafasi ya kujibu kwa uhuru. 

Katy Robjant ambaye anafanya kazi na wahasiriwa wa ukatili wa kijinsia katika migogoro nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo na maeneo mengine ana ushauri huu maalum kwa waandishi wa habari:

Badala ya kuuliza maswali ya wazi kuhusu matukio kwa ujumla, hakikisha na mhojiwa wako kwamba kuna jambo maalum unatarajia kuzungumzia. Kisha muulize akuambie kadiri awezavyo kuhusu tukio au mada hiyo. Baada ya kukupa habari zote ambazo angependa kuzungumzia, kazi yako inabaki kuuliza maswali muhimu. Hii ni njia moja ya kuzuia kumlazimisha mhojiwa wako kuzungumza mambo ambayo hataki kusema au kufikiria. [a]

Ushauri kuhusu usikilizaji mzuri ni pamoja na: 

  • kuruhusu ukimya na kuwapa watu nafasi ya kufikiria 
  • kutumia  maneno au, ikiwa unarekodi, kutumia alama za ishara kuonyesha kuwa bado unamsikiza
  • kuuliza ili kuhakikisha kuwa umeelewa vidokezo muhimu
  • Kujua jinsi ya kukaa na usumbufu wako mwenyewe na kutoruhusu kuchukua mwelekeo mbali na aliyehojiwa.

Jaribu kuepuka:

  • kumaliza sentensi za mhojiwa au kukata mawazo kwa ghafla (isipokuwa kama anajisahau katika kumbukumbu – angalia sehemu ya #5).
  • kuonyesha ishara ya kumhukumu mhojiwa, kwa mfano kwa kuonyesha uso wa kutisha wakati mtu anasimulia jambo ambalo linaweza kutisha (kuonyesha wasiwasi au huruma ni sawa.) 
  • maswali kuhusu maelezo ya ndani au ya mwili
  • Kumwambia mhasiriwa kuwa unajua jinsi anavyohisi ( (inawezekana asikuamini kwa hili)

Unapaswa pia kuwa mwangalifu kuhusu kumwambia yule unamhoji kuwa umepetia mambo kama hayo au kuongea sana kuhusu historia yako. Katika hali zingine, hii inaweza kusaidia kujenga uaminifu na kukuza mazungumzo; kwa upande mwingine, inaweza kuondoa mwelekeo mbali na anayehojiwa na kumuacha akihisi kuwa matukio yao yanapuuzwa. (Hitaji la kudumisha mipaka ya kiafya limejadiliwa zaidi katika kifungu cha namba #6). 

Mpangilio wa wakati na kutamatisha vizuri

Kichwa cha sehemu hii, Kuruhusu wahasiriwa nafasi ya kuongea kwa njia na kwa wakati wanaoridhia haimaanishi kwamba huna nafasi yoyote kwenye mpangilio wa wakati. Wakati watu ni wanyonge, wananufaika na mazungumzo yakiwa na miongozo. Na kama ilivyoelezwa hapo juu, unahitaji kuangalia viwango vyao vya kuendelea kuzingatia (Ikiwa uko katika eneo hilo kwa muda mfupi unaweza kupendekeza kurudi mara nyingine ili kuendelea na mazungumzo.) 

Madaktari wengine huzungumza juu ya sheria ya theluthi tatu. Kuwa katika theluthi ya kwanza ya mazungumzo yanapaswa kuzingatia wakati na matukio ambayo mhojiwa alihisi salama; sehemu ya pili ni kwenye mazungumzo magumu zaidi, kwa mfano matukio yanayoleta kiwewe; na sehemu ya mwisho ni kuhusu maisha ya sasa na ya baadaye – chochote kinachosaidia mhasiriwa kurudi hali ya sasa. Sio vizuri kumuacha mtu mwishoni mwa mahojiano akiwa bado amezama kabisa katika yale mabaya yaliyompata. 

Jaribu kumaliza kwa njia nzuri lakini usilazimishe na kujifanya kuwa mambo ni bora kuliko yalivyo. Unaweza kumuuliza mhojiwa ni nini ameona ni muhimu katika kupambana na hali hii na nini angependekeza kwa wengine. Si rahisi kila wakati kupata namna nzuri ya kumaliza mahojiano. Kwa uchache, unaweza kumuuliza mhojiwa nini watafanya muda uliobaki siku hio. Kumbuka, kuwashukuru wahusika na kuhakikisha unatimiza ahadi zozote unazotoa kama vile, mawasiliano ya baadaye, kutuma habari kuhusu makala na kadhalika.